Monday, August 4, 2014

JITAMBUE ILI UFANYE ULIYOKUSUDIA KUYAFANYA

 Neno jitambue ni kubwa na lenye kubeba maana nyingi kwa mtu yeyote anayekutana nalo, jitambue ni hali ya mtu kujifahamu yeye ni nani na anatakiwa afanye nini katika kila eneo la maisha yake.  

Kuna watu wanatembea lakini ukiwaangalia wamekata tamaa, wamezingirwa na mawazo lukuki yanayowafanya wasiwe na mawazo mapya katika fikra zao. Wamegubikwa na mambo mengi kiasi cha kujiona kwa nini wanaishi katika ulunwengu huu.

Watu wengi wamekuwa wepesi sana kukimbilia kwa rafiki zao ili kuomba msaada wa mawazo ya nini wafanye  kwenye maisha na hasa wakati wa shida.  Imani iliyojengeka kwa wengi katika jamii yetu ni kuwa, ushauri ni kitu muhimu sana kwa kila hatua.

Unaamka umenuna, unaoga umenuna, unavaa umenuna, unakwenda kazini umenuna. Jioni unarudi umenuna! Inasaidia nini? Kama una dukuduku na mke au mumeo, mwambie. Zungumza naye. Unanuna nini? Haitakusaidia kitu. Njia njema zaidi ya kumaliza matatizo ndani ya nyumba ni mazungumzo. Chukua hili kutoka kwangu.  

Hakuna kitu kibaya maishani kama kuonekana upo katika daraja la chini na mtu wa kudharaulika kwenye jamii unayoishi. Kisaikolojia kuna madhara makubwa.

Ni imani yangu kuwa kila mwanadamu timamu anapenda kuheshimiwa lakini wengi wetu tunashindwa kupata heshima tunayoitaka kwa sababu hatufahamu jinsi ya kuishi mbele ya wenzetu.

Watu wengi wamenifuata na kuniambia kuwa hawana furaha ya maisha. Niliwauliza kwa nini hawana furaha? Bila kusita kila mtu aliniorodheshea wingi wa shida zinazomkabili ambazo kwa namna moja au nyingine zimemfanya akose raha.

Lakini, je, kuwa na shida au mahitaji ya fedha ya matumizi, kuachwa na mume au kufiwa ni lazima iwe sababu ya mtu kukosa furaha? Mbona kuna wengine wanafurahia ujane kwa sababu tu wamebaki na mali za urithi?

Siku zote kikwazo cha furaha ya mwanadamu ni watu ingawa mazingira nayo huchangia kwa kiasi fulani lakini binadamu wenzake ndiyo adui namba moja wa raha ya mtu.

Tunaweza kujiuliza kwa nini watu ni tatizo? Jibu ni ni jepesi, mwanadamu hawezi kujihukumu kama hakuhukumiwa na wenzake. Katika hali ya kawaida, ukosefu wa furaha husababishwa na hukumu za watu ambazo huleta mawazo yanayoweza kumfanya mtu ajione duni.

Kitaalamu, ile hali ya kujiona mtu wa hali ya chini, uliyeshindwa kufanikiwa katika hili, uliyepitwa na wenzako kwa uwezo fulani, ndiyo huleta hali ya kukosa raha. Hii ina maana kuwa kukosa chakula chenye chumvi nyikani kusikokuwa na watu hakuwezi kukukosesha furaha kwa namna yoyote kama tu mawazo yako yanautetea udhaifu wako. 

Tabia kuu ya mwanadamu ni ulinganifu na wenzake, kile ambacho anaamini hajakipata ila mwenzake anacho ndicho huwa kikwazo cha furaha yake.  Hii ina maana kwamba tabia ya mtu kuwaza jinsi binadamu wenzake wanavyomfikiria ndiyo kisa ambacho humuondolea furaha.

Wakati wote tabia ya watu wasiokuwa na furaha huwa ni kufikiri namna ambavyo wenzake wanamfikiria. “Nimeshindwa kuendeleza duka langu, wenzagu si watanicheka?” Mawazo ya namna hii ya kuona wewe ni sehemu ya wale ndiyo mfereji wa kupoteza furaha yako.

Kwa kawaida, binadamu anapojifikiri mwenyewe bila kujilinganisha na wenzake hukubaliana na udhaifu wake na hilo haliwezi kuwa chanzo cha yeye kupoteza furaha yake.

Adamu na Hawa, wazazi wa kwanza wa binadamu kwa mujibu wa kitabu cha Biblia, hawakuuona udhaifu wao walipokuwa wakijifikiria wenyewe na nafsi zao mpaka nyoka alipowaletea mawazo ya kuazima kutoka kwa mtu mwingine ambayo yaliwageuza na kujiona wanyonge, wakatamani kuwa kama mtu.

Inaelezwa kwenye kitabu hicho kuwa, nyoka aliwauliza kama wanakubaliana na katazo la kutokula tunda la mti wa uzima ambapo wao walisema NDIYO, lakini waliporithishwa mawazo kuwa kuna mwingine anayewazidi ufahamu, waligeuka na kujiona wanyonge, wasiokuwa na utimilifu, wakosefu wa furaha na hivyo kuamua kula tunda si kwa sababu walipenda bali walitamani kufanana na mtu mwingine.

Ushauri wangu: Kama mtu anataka kuwa na furaha ya maisha anatakiwa kujifikiria zaidi mwenyewe na kuepukana na tabia za kukopa utu wa mwingine na kutamani kufanana naye. Mtu unaweza kuugua kwa muda, ukitulia utapona, unaweza kuwa maskini, lakini ukiacha kukata tamaa na kuongeza bidii utatajirika, hayo ndiyo maisha.

Kukosekana kwa jambo fulani unalolihitaji leo haina maana utu wako umepungua bali ni mapito ya maisha ambayo unatakiwa kukabiliana nayo wewe mwenyewe na mawazo yako na kuzishinda changamoto zote.

Kama ni mawazo ya kuazima basi lazima yawe yale ya kukusaidia mbinu za kushinda na si yatakayokufanya kujiona dhaifu mbele ya binadamu wenzako. Jipe moyo ushindi wa hayo yanayokukosesha furaha upo mikononi na akilini mwako.

Ni imani yangu kuwa kila mwanadamu timamu anapenda kuheshimiwa lakini wengi wetu tunashindwa kupata heshima tunayoitaka kwa sababu hatufahamu jinsi ya kuishi mbele ya wenzetu.

Kitaalamu, hakuna jambo ambalo hutokea maishani bila sababu maalumu hivyo hata kudharauliwa kwako au kwetu ndani ya jamii tunayoishi kunatokana na jinsi tunavyoenenda.

Watu waliopitia matatizo na shida duniani wameorodhesha  mambo mengi yaliyowafanya wawe kama walivyo, walipitia shida, walifeli, walishindwa na baadae wakajitambua na kuinuka na kuanza upya haujachelewa simama na anza tena utashangaa na kuwa ushuhuda kwa watu wengine. 

Watu wengi wanayaona mafanikio kwa watu weupe tu hapana, hata wewe unaweza kufanikiwa ukijitambua na ukiishi katika mtazamo wako na wala sio mtazamo wa mtu mwingine kwani kila mtu ana wazo lake na ana kipawa chake alichojaaliwa na Mungu na ndio maana unaweza kuiga mtu kuuza vitumbua kumbe sio karama yako kesho yake unaacha kwa kukosa uvumilivu wa kuungua na moto na harufu ya mafuta.

Simama katika nafasi yako na amua kuishi kwa jinsi unavyotaka wewe huku ukiwa na malengo yenye dhima ya kufikia ushindi wa hali ya juu sana.

Hakuna kinachotokea kwenye maisha yako bila kuwa na sababu, umezaliwa ili upambane na kufikia kilele cha hatima yako na siku zako za kuishi anajua yeye aliyekuleta hapa duniani.  Na mwisho wa siku zitatakiwa hesabu zake. Utaulizwa ulifanya nini kule ulikokwenda yaani hapa duniani.

 Ebu yaangalie haya hapa chini na kuyafanyia kazi kama unataka kujitambua na kuwa mahali pa kuheshimika katika jamii inayokuzunguka:-

MUONEKANO
Kwanza kabisa ni jinsi unavyoonekana. Muonekano ninaouzungumzia hapa ni usafi wa mavazi na mwili kwa ujumla. Hata siku moja hakuna mchafu anayeheshimika katika jamii anayoishi hata kama ana kipaji kikubwa kiasi gani.

Kwa hiyo uchafu wa mavazi na mwili huchangia mtu kudharauliwa katika jamii anayoishi. Linaweza kuwa jambo dogo sana lakini ni moja kati ya sababu kubwa inayochangia kuporomoka kwa thamani yako mbele ya wenzako.

Mazungumzo
Hapa naomba nieleweke kuwa unachokizungumza kinaweza kukujengea heshima au kukubomolea heshima. Kauli zisizo na busara zitakufanya udharaulike kwa kila mtu. Uropokaji usiokuwa na mantiki huchangia kuporomosha heshima yako hasa kama utakuwa muongeaji zaidi. Biblia inasema penye wingi wa maneno hapakosi uovu.

UTENDAKAZI WAKO
Ndugu zangu, siku zote heshima ya mtu ni kazi. Watu wengi hawapendi kufanya kazi kwa bidii huku wengine wakijiendekeza kwa tabia ya kuombaomba, jambo hilo halifai kwa vile huchangia kubomoa heshima yako mbele ya jamii. Fanya kazi usiishi bila kujishughulisha.

KUTOTIMIZA AHADI
Kama una tabia za kuahidi mambo halafu unashindwa kuyatekeleza, basi unajiweka katika nafasi mbaya ya kutunza heshima yako katika jamii unayoishi. Bora ukwepe kutoa ahadi kuliko kuahidi na kutotimiza.

SIFA ZISIZO NA MAANA
Nakumbuka msemo mmoja kutoka kwa mwandishi mwandamizi aliyekuwa mtaalamu wa falsafa za maisha, marehemu Adolf Balingilaki, ambao unasema kwamba:
“Ukitafuta heshima kwa gharama ya juu, basi utalipwa dharau kwa bei nafuu.”
Msemo huu unamaanisha nini? Siku zote ukiwa unafanya mambo yako kwa ajili ya kusifiwa au mazungumzo yako kuwa ya kujiinua, watu watakudharau.

KUTOKUWA MWAMINIFU
Suala la uaminifu ni pana, kuna uaminifu wa fedha, siri, dhamana na mambo kama hayo, hivyo ni vema kila unachoaminiwa lazima ukitunze kwani ukiwa mtu wa kuvunja uaminifu fahamu kuwa utashusha heshima yako.

Karibu tuelimishane na kusaidia pale unapojua niko tayari kujifunza toka kwako; naamini ili niweze kujua zaidi natakiwa kujifunza kupitia wenzangu.  

Karibuni sana tusonge mbele kwa ushindi.

Lusako Mwakiluma

No comments:

Post a Comment