Monday, June 23, 2014

KILA KIZUIZI KATIKA MAISHA YAKO KINA UTAJIRI NDANI YAKE




Mimi sidhani  kama kuna nguvu  yoyote ya mafanikio duniani, zaidi ya maneno haya “ katika mafanikio  duniani ni zaidi ya kujidhatiti na kutokata tamaa”.  Maisha ya kutokana tamaa  yanashinda  kila kizuizi cha  hapa duniani, hata nguvu  zozote za kiasili”  Bwana John D. Rockfeller, alizaliwa mwaka 1839 – kufariki 1937; alikuta baba yake na ukoo wake ni wa kimaskini.  Zaidi baba yake  mwenyewe hakuwa na muda na mtoto wake, katika kukaa kwake John alijitengenezea  njia zake mwenyewe kwa mfumo wake mwenyewe.  Hakusema eti… familia yetu ni maskini … oh ukoo wangu ni maskini.  Alisimama yeye kama yeye na kufanya kazi kwa bidii na alikuwa mwanamapinduzi wa viwanda duniani.

Na wewe unapokutana na vikwazo katika maisha yako simama katika nafasi yako jitahidi uvishinde ili uweze kwenda upande wa pili, kila kikwazo kina maana na ndio maana kuna mitihani ambayo inatusababishia kuvuka daraja na kwenda mbele, mitihani isingekuwepo tusingeweza kusoma shule.  Na majaribu yasingekuwepo watu wangeridhika na hali walizonazo.  Mtu akipitia majaribu na changamoto anakuwa mwalimu mzuri sana kwa mwingine.  Kumbuka kila tatizo unalopitia kuna mtu mwingine aliwahi kupitia kabla yako unatakiwa uwe makini na kuweza kuwahoji watu jinsi ya kutatua matatizo unapoona kuna ugumu wa aina ya tofauti.

Na ukiona mambo ni rahisi wakati wote basi ujue haupigi hatua yoyote katika maisha yako unakuwa mtu wa kuridhika siku zote.  Wapo watu wengi sana waliofanikiwa kuweka rekodi ya dunia, ambao ni  mashujaa wakubwa  wa dunia, na si kwamba walikuta  maisha ni matamu kuyaishi  ila waliamua  kuyatengeneza maisha yao kwa mifumo yao.  Akina Frederick Douglas, tena ndugu huyu alisema maneno haya “Ukiamua  kuyakubali maisha ya kawaida kwa  kutumia uwezo wa kawaida hata kama  ukipata fursa ya maisha utajikuta  ukifanya kazi na kufanya kazi zote za miaka ya maisha yako yote mpaka  unakufa maskini”.  Fanya  zaidi ya kawaida.  Nenda zaidi ya mazoea.

Nakubaliana na kauli ya Rais Mweusi wa kwanza wa Marekani, Barack Obama aliyesema maneno haya “Kutengeneza alama yako duniani ni kazi, lazima ulipie  gharama”.   Lazima  upambane, lazima upigane  bila kuvunjika moyo.  Kama ingekuwa rahisi kila binadamu angefanya lakini inawezekana kwa kila binadamu yeyote  atakayeamua  kujidhatiti na kuvumilia kwani ukiwa njiani kuyafikia haya utasukumwa na vizuizi vya kila aina na hata kuanguka mara kadhaa.  Jambo la muhimu ni kuingia na kuyafanya uyatakayo duniani na si kukimbia kuangushwa njiani, kubali kujifunza  na kukomazwa na magumu unayoyapitia kwa kuchukua  hatua katika  kila muda unapoangushwa au unaweza  kujiaibisha mwenyewe  kwa kutochukua  hatua na kurudi nyuma baada ya kuangushwa au ukaamua  kupigana na kupigana mpaka unajifunza  kupitia hayo na  mwisho unapata yale uyatakayo duniani.  Tukumbuke  maisha ni mara moja duniani, hatutaishi tena na jinsi tulivyo sasa”.

Kubali vikwazo, ruka vihunzi ili uweze kwenda hatua nyingine mbele yako.
Na Lusako Mwakiluma

No comments:

Post a Comment