Wednesday, May 28, 2014

MAISHA YA FAMILIA





Naomba tutafakari zaidi na zaidi kuhusu maisha ya familia kwani uhai wa familia ni uhai wa Kanisa na taifa zima la Mungu. Maisha ya familia ni zawadi kubwa ambayo Mungu ametujalia tangu pale alipoumba ulimwengu kwani yeye aliona kuwa “si vema huyu mtu awe peke yake, nitamfanyizia msaidizi wa kufanana naye” (Mwanzo 2:18). 

Hapa tunaona hekima ya Mungu ya kumuumba mume na mke na kuwaambia kuwa “Kwa hiyo mwanaume atamwacha baba yake na mama yake naye ataambatana na mkewe, nao watakuwa mwili mmoja” (Mwanzo 2:24). Tunaishi katika ulimwengu wenye changamoto nyingi ambazo tusipokuwa macho zinaweza kuhatarisha ule umoja kati ya mume na mke, umoja ambao Mwenyezi Mungu anatuambia kuwa “Mwanadamu asiutenganishe”.

Tunapoendelea kutafakari kuhusu maisha ya familia na changamoto zake katika ulimwengu wa utandawazi, sayansi na teknolojia, leo hii ningependa tutafari pamoja kuhusu tatizo la kuvunjika kwa Agano la ndoa kati ya Mume na Mke katika jamii zetu. Jambo hili linaonekana kama kitu cha kawaida katika ulimwengu wetu wa leo. 

Kadiri ya Mafundisho ya Kanisa ambayo msingi wake ni Maandiko Matakatifu kama tulivyoona, Agano la Ndoa Takatifu ambalo linatambulika na Kanisa kama Sakramenti linaweza kutenganishwa na Mungu pekee pale kinapotekea kifo cha mwenzi mmoja wapo. Hivyo basi, pale wenzi wawili(Mume na Mke) wanaposema kuwa wanapendana kwa dhati, upendo huo sio upendo wa majaribio bali ni upendo unaowaalika wapenzi hao wawili kila mmoja kujitoa kwa mwenzake mzima mzima bila kujibakisha. 

Hii hali ya kijotoa kwa mwingine ni sadaka kubwa katika maisha kwani wapenzi hawa wanakubali kupokeana kama walivyo katika raha na taabu, maana yake wanakubali kusaidiana kuubeba msalaba wa maisha katika mazingira yoyote kwa lengo la kuupata utakatifu.

Na Lusako Mwakiluma

No comments:

Post a Comment